03/11/2013
Sitta Tumma
“KWA sasa, hisa za Benki yetu ya Mwanza Community zinanunuliwa kwa wingi sana...na tumeanza hivi karibuni lakini hadi sasa tumeshauza hisa 600,000.
“Hisa moja tunauza sh 550 tu, ni vizuri sana wananchi wakachangamkia fursa hii.”
Hiyo ni kauli ya Mwenyekiti wa Kamati ya Uanzilishi wa Mwanza Community Benki (PLC), Joseph Kahungwa, anayoitoa wakati akizungumzia mkakati wa uanzishwaji wa benki hiyo jijini hapa.
Kahungwa anasema: “Ingawa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), imetupa sharti la kuuza hisa za hadi sh bilioni 2.1 ndiyo itupe leseni, lakini kwa jinsi watu wanavyojitokeza kununua kwa kasi hisa zetu hadi mwishoni mwa Oktoba mwaka huu, zitakuwa zimefikia lengo.”
Kuanzishwa kwa benki hiyo ambayo kwa sasa ipo kwenye kasi ya kuuza hisa kwa wananchi imelenga kuinua pato la kiuchumi la wananchi.
Katika harakati za kufikia malengo iliyopewa na BoT ya kukusanya hisa za sh bilioni 2.1 ndipo ipewe leseni la kusimama katika ushindani wa kibenki, tayari uuzaji wa hisa hizo kwa sasa umeshika kasi zaidi.
Kwa mujibu wa Kahungwa, ipo k**ati iliyoundwa maalumu kwa ajili ya uanzishaji wa benki hiyo, kwa sasa ina mtaji wa sh milioni 340.
Jumla ya hisa za sh milioni tano zinahitajika kuuzwa ili kuwa na mtaji wa sh bilioni 2.75. Pesa hizi ni zaidi ya lengo la BoT.
“Kwa kweli watu wamechangamkia sana kununua hisa za benki yetu. Na kila mwananchi anayenunua hisa anakuwa ni sehemu ya mmiliki halali wa Mwanza Community Benki.
“Kwa maana hiyo, hadi sasa zaidi ya hisa 600,000 tumeshauza kwa kipindi kifupi…hii inatokana na jinsi wananchi walivyohamasika na kufahamu umuhimu wa kumiliki uchumi wao,” anasisitiza Kahungwa.
Anasema kwa kuwa hisa moja inauzwa sh 550; hivyo kiwango cha chini mtu yeyote kununua ni hisa 100 zitakazogharimu sh 55,000.
Kwa mujibu wa Kahungwa, hisa za benki hiyo zinauzwa kwenye Benki za Azania na Posta pamoja na Mwanza Community Benki.
“Wanaoruhusiwa kununua hisa za benki yetu ni raia wa Tanzania na wasiokuwa raia…lakini mtu mwenye umri chini ya miaka 18 anaruhusiwa kununua ila sharti awe na mdhamini,” anafafanua mwenyekiti huyo wa k**ati ya uanzilishi wa benki hiyo.
Kwa sasa Mkoa wa Mwanza unatajwa kukua kiuchumi na umekuwa zaidi kutoka asilimia 7 ya awali.
Shughuli za kiuchumi na usalama ni moja ya vitu vinavyochangia Mwanza ing’are kiuchumi.
Kwa sasa matawi ya benki jijini hapa yanakadiriwa kufikia zaidi ya 12. Hii nayo ni fursa maalumu ya pato la kiuchumi kuongezeka maradufu Mwanza.
Ujio wa Mwanza Community Benki ni kichocheo kikubwa pia cha kukuza uchumi wa Mwanza na raia wake.
Akitoa mchanganuo kuhusu takwimu za hisa zinazotakiwa kuuzwa, Kahungwa hapa anasema wanahisa waanzilishi tayari wameshanunua hisa 600,000 sawa na asilimia 12, huku zinazotakiwa kuuzwa kwa umma ni hisa 4,400,000, sawa na asilimia 88.
Kwa maana hiyo, ukichukua hisa za waanzilishi 600,000 ukajumlisha na hisa 4,400,000 zinazotakiwa kuuzwa kwa wananchi, utapata jumla ya hisa milioni tano zinazofikisha kiasi cha sh bilioni 2.57.
Mwenyekiti huyo anawasihi wananchi kuchangamkia fursa ya ununuzi wa hisa hizo ili kuwa miongoni mwa wamiliki wa benki hiyo mpya.
Mkuu wa Mkoa (RC) wa Mwanza, Injinia Evarist Ndikilo anathibitisha kwamba ujio wa benki hiyo ni chachu kubwa katika uchumi wa wananchi wa mkoa wake huo.
Anasema wananchi wengi ni vema wakajitokeza haraka kununua hisa za benki hiyo kwani hiyo ni moja ya njia ya kujipanga na kujiwezesha kumiliki uchumi mkubwa kuanzia hivi sasa na siku zijazo.
“Ujio wa hii Mwanza Community Benki ni fursa nzuri sana tena kwa wakazi wa Mwanza na mikoa jirani kuanza kumiliki uchumi mkubwa. Nawasihi sana wanunue hisa nyingi na mapema zaidi kabla ya Oktoba 31, mwaka huu,” anasema Ndikilo.
Ndikilo anafafanua kwamba kiwango cha sh 550 kwa hisa moja zinazouzwa na Mwanza Community Benki ni kidogo mno na kinamwezesha kila mwananchi kununua hisa zaidi ya 100.
Anasema: “Ukinunua hisa zako hata 5,000, 8,000, 15,000 au zaidi ya hapo, si utakuwa na mtaji mzuri sana kwenye benki hii? Hata k**a una uwezo wa kununua hisa 100, njoo ununue,” anasema.
Ndikilo anaziomba halmashauri zote mkoani hapa kuchangia katika harakati za maendeleo ya benki hiyo na anauomba uongozi wa Mwanza Community Benki kuzishirikisha kampuni na mashirika yote yaliyopo Mwanza ili kufikia malengo halisi.
Kimsingi Mwanza na mikoa jirani ya Kanda ya Ziwa huu ni mwanya wao wa kununua hisa katika benki hiyo.
Hisa hizo zitawawezesha kuwa na uchumi na wamiliki wa benki husika.
Upo umuhimu wa jamii kuchangamkia fursa hiyo, maana kwa jinsi kasi kubwa ya ununuzi wa hisa hizo unavyofanyika kwa wananchi, ni dhahiri kwamba hadi kufikia Oktoba 31, mwaka huu ambapo ndiyo mwisho wa uuzaji, idadi ya hisa milioni tano zenye thamani ya sh bilioni 2.75 zitakuwa zimeuzwa.
+255 784 785294 +255 754 568142 [email protected] au [email protected]