12/07/2025
Benki ya Biashara DCB imeshiriki rasmi katika Siku Maalum ya Dar es Salaam (DSM Day 2025) yaliyofanyika tarehe 10 Julai 2025, katika Ukumbi wa Ali Hassan Mwinyi ndani ya Maonesho ya 49 ya Kimataifa ya Biashara (Sabasaba). Ushiriki huu umetokana na mwaliko rasmi kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila. Tukio hili limewakutanisha viongozi wa serikali, wawekezaji, taasisi za kifedha na wadau mbalimbali kwa lengo la kujadili fursa za maendeleo na uwekezaji ndani ya jiji la Dar es Salaam.
Kupitia ushiriki huu, DCB ilipata fursa ya kuonesha huduma na bidhaa zake za kifedha, kutoa elimu ya fedha kwa wananchi, na kushiriki mijadala kuhusu namna taasisi za kifedha zinavyoweza kuchangia katika ustawi wa jamii na uchumi wa mkoa. Ushiriki wa DCB unaonesha dhamira ya benki kuendelea kuwa mshirika wa karibu wa maendeleo, kuhakikisha huduma jumuishi, bora na zenye tija zinawafikia Watanzania wote.